Arudi shule baada ya utafiti wa TAMWA




UTAFITI wa kihabari uliofanywa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), Machi 2012 umefanikisha kumrudisha shuleni mwanafunzi wa sekondari aliyekuwa ametelekezwa yeye pamoja na familia yao.

Mwenjuma Magalu ambaye kwa sasa ni mwanafunzi wa kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Komnyang'anyo alitelekezwa na babayake yeye pamoja na mamayake mwaka jana, hivyo kushindwa kujiunga na kidato cha kwanza katika shule hiyo licha ya kuchanguliwa kuendelea na masomo.

Hata hivyo baada ya utafiti wa kihabari kufanyika kijijini Msasa Wilaya ya Handeni na taarifa za mtoto huyo kushindwa kujiunga na sekondari baada ya mamayake (kwa sasa marehemu) kukosa uwezo kuripotiwa, alijitokeza mfadhili wa kumsomesha ambaye anagharamia masomo yake hadi sasa.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi juzi akiwa shuleni Komnyang'anyo, mwanafunzi huyo aliishukuru TAMWA kwa kuibua tatizo la familia yao kwa umma na kupatikana kwa mfadhili ambaye amemrudisha masomoni licha ya familia yao kutelekezwa.

"Binafsi nawashukuru sana hao (TAMWA) waliopaza sauti hadi mjuu wangu kurudi shuleni...hii kwetu ilikuwa ni ndoto kwetu maana mtoto mwenyewe alikuwa amekata tamaa kabisa kurudi shuleni na alikuwa kaanza kufanya vibarua mitaani huku wenzake wakiendelea na shule," alisema bibi wa mtoto huyo, Amina Mohamed akizungumza.

Bibi huyo akizungumzia maisha ya sasa ya familia hiyo alisema bado wanahitaji msaada wa huduma hasa baada ya mwanaye kufariki dunia mwaka jana na kumuachia watoto wake.

Aliongeza kwa sasa yeye ni mgonjwa wa TB anayetumia dawa hivyo kwa hali yake ameshauriwa kupumzika jambo ambalo limempa mzigo mkubwa kimajukumu mwanafunzi (Mwenjuma), kufanya kazi za nymbani kama kupika kulima na shughuli nyingine.


Hata hivyo mama wa mtoto huyo (Hadija Magalu) ambaye alitelekezwa na mzazi mwenzake alifariki dunia mwaka jana kwa tatizo la uzazi na kuiacha tena familia hiyo ya watoto watatu katika hali ngumu zaidi chini ya malezi ya bibi mzaa mama.

kwa hisani ya mjengwablog

No comments: